Watu wengi wametambua na kuanza fursa ya kutengeneza mamilioni kwa kuendesha abiria kwenye majukwaa ya safari kama Uber na Bolt. Lakini je? Ni kila mtu anaweza kutengeneza kipato cha kutosha kwa njia hii?
Madereva wengi hasa wale wapya huanza kazi hii bila kujifunza misingi muhimu zaidi ya kuwafanya wafanikiwe. Kama wewe ni dereva au mmiliki gari okoa muda na uanze kutengeneza pesa barabarani kwa kufata maelekezo yafuatayo
1. PATA TIPS KWA KUWA MSTAARABU
Ukipita kwenye mitandao ya jamii utakutana na stori za jinsi abiria wengi wanavyokutana na madereva wenye kauli na huduma mbaya zinazowapelekea kuchukia safari.
Kila mtu ana matatizo yake katika maisha. Jambo jema ni kuhakikisha kwa ule muda mfupi ambao abiria wako anakuwa kwenye gari lako unampokea na kuongea naye vizuri ili awe na amani.
Pia ni muhimu kuwa mtanashati na kuonekana proffessional. Hii hufanya abiria wafurahie huduma yako hivyo kukupa tips kubwa au nyongeza kama shukrani.
2. ONGELEA EXPERIENCE YAKO KWENYE YOUTUBE AU BLOG
Watu wengi wangetamani kutengeneza pesa kwa kuendesha abiria kwenye uber au bolt lakini wanakosa taarifa sahihi. Ili kutengeneza fedha ya ziada unaweza kuongelea au kuwafundisha kwa kupitia video, maandishi(blog) au sauti (podcast) na ukatengeneza pesa zaidi kupitia majukwaa yao.
3. PATA FURSA KUTOKA KWA WATEJA
Kila siku mpya ni fursa mpya ya kujifunza kitu kipya. Abiria wako anaweza kuwa mtu yeyote yule ambaye ana uwezo wa kukuunganisha na njia nyingine za kutengeneza pesa zaidi.
Kwa hiyo jitahidi kuongea nao vizuri na kutengeneza mahusiano mazuri kiasi kwamba wanaweza kukushauri, kukuelimisha au kukupa fursa nyingine mbali na hii.
4. OKOA GHARAMA YA MAFUTA
Ili kutengeneza faida ni muhimu kupunguza matumizi. Unaweza kupunguza gharama ya mafuta kwa njia kama zifuatazo:
- Nunua mafuta kwenye sheli zenye gharama ndogo zaidi: Hata kama tofauti ni sh 200.
- Punguza matumizi ya kiyoyozi (Air conditioner)
- Epuka kuhama hama kufata sehemu zenye wateja wengi mara baada ya kushusha abiria.
5. ZINGATIA MAENEO NA MUDA WENYE ABIRIA WENGI
Fanya uchunguzi na uyajue yale maeneo ambayo watu wengi huitisha Uber / Bolt na uanze kuendesha huko. Pia chunguza ni wakati upi katika siku watu wengi zaidi wanahitaji huduma ya usafiri. Hii itasaidia sana katika kutengeneza pesa zaidi kwasababu utakuwa na abiria kila saa.
Usijali kama vile wewe sio mwenyeji wa maeneo hayo kwasabu ni rahisi kujifunza hasa kwasababu ya matumizi ya gps. Pia mtu mmoja hawezi kujigawa na kuendesha katika maeneo yote maarufu kwa wateja. Jitahidi kuchagua maeneo machache ambayo utayamudu.
6. FATA NYUMBA ZA STAREHE
Kama unataka kutengeneza pesa nyingi kwenye Uber au Bolt basi hakikisha unafahamu sehemu maarufu ambazo zinauza pombe.
Watu wengi hupenda kujumuika sehemu hizi na wengi hawapendi kuendesha baada ya kunywa pombe hivyo uhitaji wa usafiri unakuwa juu hasa wakati wa mwisho wa wiki yaani Ijumaa hadi jumapili.
7. ENDESHA MUDA AMBAO WENGI HAWAENDESHI

Kadri siku zinavyozidi kwenda ndivyo watu wanavyozidi kutambua fursa ya kutengeneza fedha na Uber / Bolt hivyo kuleta ongezeko la madereva.
Kwa hiyo ili kutengeneza pesa zaidi ni muhimu kufanya kazi wakati wengine wamepumzika ili kupunguza ushindani wa soko. Siku za weekend zinaweza kuonekana kuwa ndio nzuri zaidi kutengeneza fedha lakini kila mtu analifahamu hili kwa hiyo madereva wengi wanakuwa wanaendesha.
Muda mzuri zaidi ambao huwa na madereva wachache ni kama saa tisa hadi saa moja asubuhi.
7. ENDESHA SIKU ZA SIKUKUU NA MATUKIO MAKUBWA
Siku za sikukuu zina wateja wengi kwasabau watu wanapendelea zaidi kwenda sehemu za kupumzika. Pia hiki ndicho kipindi watu wengi wanasafiri kwa hiyo trip za kwenda na kurudi stendi au airport zinakuwa nyingi zaidi. Hakikisha unakumbuka tarehe zote za sikukuu na unajiandaa mapema kupata abiria.
Chunguza pia siku ambazo zina matukio kama matamasha, concert za muziki, mikutano mikubwa (conferences), send off, harusi nk.
Siku hizi zina watu wengi ambao wanaenda kwenye sehemu ya tukio kila siku kwa muda wa siku fulani. Ukifahamu matukio yalipo utaweza kupata wateja kirahisi na kutengeneza pesa nyingi zaidi.
8. BADILISHA MAAMUZI YA WATEJA WAKO
Unapoongea vizuri na abiria na wakakuambia kuhusu wanapoelekea, unao uwezo wa kuwashauri sehemu nzuri zaidi au njia nzuri zaidi hivyo kuwafanya waongeze safari na gharama kuongezeka.
Pia kama hawakai hapo kwa muda mrefu au kama watakuambia muda wanaotegemea kurudi basi unakuwa na uhakika wa kupata trip nyingine ya kuwarudisha kwasababu tayari wanakuamini.
9. UZA MAHITAJI MUHIMU

Kwa barabara zetu za Daresalaam safari fupi inaweza kugeuka kuwa safari ndefu ghafla kutokana na foleni, kufungwa barabara nk. Abiria wako wanaweza kupata kiu, njaa au wanaweza kuwa wamesahau au wamepoteza charger nk.
Tengeneza pesa zaidi kwa kuweka tray nzuri yenye bidhaa kama vifuatazo:
- Vinywaji kama maji, energy drinks na soda.
- Charger za simu na headphones.
- Miamvuli wakati wa mvua na jua kali.
Ni muhimu kuwa na kisehemu cha kuviweka ili wateja wakiingia tu wanaviona na wanavitamani. Vitu hivi pia vitauzika sana hata usiku wa manane ambapo hakuna foleni kwasababu, wateja wa usiku wanakuwa wametoka kunywa pombe au kucheza muziki hivyo kuwa na kiu na njaa sana.
10. ENDESHA KWENYE MAJUKWAA TOFAUTI
Ili kupata wateja wengi zaidi ni vizuri kujisajili kuendesha kote kwenye uber, bolt na hata kwa wateja wengine binafsi kama mahotelini kudeliver bidhaa na chakula kwa wateja. Hii itasaidia ule wakati kunapokuwa hakua wateja kwenye upande mmoja uweze kupata kwenye upande mwingine.
11. JIBRAND KWA AINA YA KIPEKEE

Ili kuhakikisha unajenga mahusiano na abiria jiweke kitofauti na madereva wengine. Tengeneza business cards ugawe, promote biashara au huduma zako nyingine kwa abiria na kwa wafanyabiashara. Ipo siku watu wenye kadi yako watakutafuta tu kwa huduma zaidi zenye malipo zaidi!
Mfano unaweza kupata wateja wanaohitaji watoto kufatwa shuleni kila siku, kupeleka wagonjwa hospitali au wamama clinic nk. Zipo fursa nyingi sana za kutengeneza pesa zaidi ukiwa wa aina yake.
Kwa kifupi: Kuwa wa kipekee fanya kazi kwa kutumia akili badala ya nguvu nyingi.
Ukiweza kufata njia hizi bila shaka utatengeneza fedha nyingi kwa kuendesha abiria kwenye Uber au Bolt.
Zingatia sana afya ya mwili wako kwa kulala masaa sahihi (6-8), kunywa maji, kula chakula kwa muda sahihi na kufanya mazoezi au kujinyoosha. Ukiwa na afya njema utatengeneza fedha kwa ufanisi zaidi.
Nimeanza kujifunza kupitia makala zako but why magari pekee🙏
Tumefurahi sana Shaka kwamba unajifunza kupitia makala zetu kwani kufanikisha hili ndio dhumuni letu kuu.
Team ya Weibak inaanda mambo mengi mazuri kwa ajili ya wadau kama wewe.
Tafadhali endelea kufuatilia tovuti yetu pamoja na mitandao ya kijamii kwa ajili ya mambo mengi mazuri tunayo tarajia kuwaletea.
Aiseee nimejifunza vtu vingi toka kwako asante mungu akbariki saaana sema. Nn changamoto ni nyngi mno endelea kutupa elimu
Tumefurahi sana kusikia hivyo kutoka kwako Benny.
Pingback: PROMOTION ZA UBER QUEST: TENGENEZA PESA ZAIDI! -