Madereva wengi wa Uber wanafahamu jinsi ya kuanza na kumaliza safarii lakini hawafahamu jinsi ya kuchagua maeneo wanayotaka wao kufanya shughuli yao ya uendeshaji.
Jukwaa la Uber lina kipengele muhimu sana kinachoitwa “Destination ride request filter” ambacho kina faida kubwa sana kwa madereva.
Hii ni kwasababu, kwa kutumia kipengele hiki unaweza kuamua kuwa safari zako zote ziishie eneo fulani tu hivyo kuzuia Uber kukutaarifu kuhusu abiria ambao hawaelekei kwenye eneo hilo.
FAIDA ZA DESTINATION FILTER KWA MADEREVA
1. UWEZO WA KUENDESHA KWENYE MAENEO UNAYOYAFAHAMU TU.
Siku zote inashauriwa kupeleka abiria kwenye maeneo unayoyafahamu vizuri kwasababu inakuwa rahisi zaidi kwako kujua hali ya barabara, mitaa na sehemu za kuegesha gari.
Unapokuwa haujaweka kikomo cha maeneo kwa kutumia filter ya Uber, una uwezekano mkubwa wa kupata abiria ambaye anaelekea eneo ambalo haulifahamu vizuri hivyo kuweza kukuletea kero wewe na abiria pia.
SOMA: Mbinu za usalama kwa madereva wanaoendesha abiria usiku.
2. INAONGEZA ACCEPTANCE RATE
Unapoweka kikomo cha maeneo ya kupeleka abiria application itakuhakikisha kuwa kila safari unayopata inaishia ndani ya eneo unalolitaka. Hii huepusha na kupunguza ishu ya dereva ku-cancel safari kwasababu abiria anaenda mbali sana au eneo ambalo haulifahamu vizuri.
Madereva wenye acceptance rate kubwa hupata abiria kiurahisi zaidi kuliko madereva wasio na alama ya juu.
Kumbuka kwamba unapoweka kikomo cha maeneo ya kupeleka abiria una uwezekano mkubwa wa kupunguza kipato kwasababu utakuwa hauwezi kuona maombi ya safari za nje ya eneo ulilochagua.
3. KUPATA SAFARI ZA KARIBU NA NYUMBANI
Destination filter ni kipengele ambacho kiliongezwa katika application ya Uber ili kusaidia madereva kupata abiria wakati wanapoamua kurudi nyumbani kupumzika.
Badala ya kurudi nyumbani na gari tupu, madereva wanaweza kuset location ya karibu na nyumbani kwao kwenye destination filter ili kupata abiria wa kwenda naye na kutengeneza pesa.
JINSI YA KUCHAGUA MAENEO YA KUPELEKA ABIRIA WA UBER
1. FUNGUA APP YA DEREVA
Bonyeza alama ya kikoo cha kukuza (magnifying glass/search) iliyopo upande wa juu kushoto ukishafungua app.
2. CHAGUA ENEO UNALOTAKA SAFARI ZAKO ZIISHIE
Ukishabonyesha magnifying glass bonyeza kipengele cha “Filter trips towards” kisha chagua “set destination”.
Baada ya hapo anza kuandika jina la eneo ambalo unataka upate safari za kwenda huko tu. Jina likitokea bonyeza “set destination” na usubiri kuona bango linalosema “destination set”.
Baada ya hapa ikitokea abiria akaomba usafiri wa kuelekea eneo ulilolichagua basi Utapata ujumbe kuwa safari fulani inaelekea kwenye eneo lako.
Kwa mfano wewe unataka kupeleka abiria mlimani city mall tu. Weka destination yako kama mlimani city na utapata taarifa abiria wakiomba safari za kuelekea hapo tu.
KUMBUKA
Si lazima kuchagua eneo dogo, unaweza kuamua kuchagua eneo kubwa mfano MWENGE. hii ina maana utapata ujumbe wa safari zote zinazoelekea sehemu yoyote ndani ya mwenge.
Hii itasaidia kuongeza uwezo wa kupata abiria wengi zaidi kwasababu eneo limekuwa kubwa zaidi.
UNAWEZA KUCHAGUA MAENEO MANGAPI?
Dereva anaweza kuchagua maeneo mawili tu ndani ya masaa 24. Hii ni muhimu kwasababu kama unapenda kuendesha kuelekea hilo eneo na kurudi ulipoanzia tu unachagua maeneo hayo mawili hivyo utakua unapeleka abiria na kurudi pale pale ulipoanzia safari.
JINSI YA KUONDOA ENEO ULILOCHAGUA
Unapochagua eneo la kuishia safari zako kwenye app yako chini kabisa kunakuwa na bango linalokukumbusha kuwa umechagua eneo la kwenda (“destination set”)
Ikitokea umeamua kuendesha tena safari kuelekea mahali popote bila kuchagua eneo maalumu, bonyeza bango hilo la “destination set”. Bonyeza jina la eneo lako ulilochagua mwanzo kisha chagua “Remove Destination”
Subiri sekunde chache hadi jina la eneo ulilochagua mwazo likishatoweka. Baada ya hapo utakuwa umerudi online na utaweza kupata maombi ya safari zozote.
Unaweza kufanya mabadiliko haya mara mbili tu katika masaa 24, kila saa sita usiku siku mpya inapoanza na wewe unakuwa na nafasi mbili za kuchagua mahala pa kupeleka abiria.
UNAWEZA KUKUBALI ABIRIA AMBAO WANASHUKIA NJIANI NA SIO PALE PALE KWENYE ENEO ULILOCHAGUA?
Kwenye jukwaa la Uber hauwezi kuona maombi ya safari ambazo hazifiki pale pale kwenye eneo ulilolichagua.
Ipo kampuni ya usafiri ambayo destination filter yake huwa inamuonesha dereva safari ambazo zinaishia njiani au zinaelekea barabara moja na eneo ulilochagua hata kama abiria hafiki kabisa kwenye eneo husika.
Kampunii hii inaitwa Lyft na hadi sasa bado haijanzisha shughuli zake nchini Tanzania. Katika jukwaa la Lyft, kwa mfano wewe dereva upo Buguruni na umechagua kupeleka abiria wa mlimani city.
Kama akitokea abiria anayeelekea Mawasiliano unaweza kuona ombi lake la safari na kumpeleka kwasababu ni njia au route ile ile ya mlimani city.
Kwa hiyo app itakutaarifu safari zote zinazoelelea njia moja au karibu na eneo ulilochagua.
Kama abiria ameomba safari ya kwenda Kimara kwa mfano, wewe hautapata ujumbe wowote wa safari kwasababu huyu haendi kwenye njia au route ya eneo ulilochagua wewe ambalo ni Mlimani city mall.
Inawezekana huko mbeleni kampuni ya Uber itaweza kuboresha kipengele hiki na kufanya madereva wanaochagua maeneo maalumu waweze kuendesha na abiria wanaoishia njiani. Lakini hii si ya kuitegemea sana kwasababu tayari Uber ina madereva wengi.
Ni muhimu sana kufahamu jinsi ya kuchagua maeneo ya kupeleka abiria wa Uber kwasababu inakupa uwezo wa kujipangia kwenda sehemu unazopenda tu au sehemu zenye matukio fulani muhimu kwa siku hiyo.
Pia ni nzur sana kwasababu pale linapotokea ombi la safari inayoishia kwenye eneo ulilochagua basi wewe ndiye utakayepewa kipaumbele na Uber kupeleka hao abiria kuliko madereva wengine.
Hii ni kwasababu unapochagua eneo maalumu unaonekana kuwa wewe ni mzoefu sana wa eneo lile kuliko madereva wengine ambao wapo tayari kwenda kokote.
JINSI YA KUAMUA ENEO LIPI UCHAGUE ILI KUPATA FEDHA NYINGI ZAIDI
UWANJA WA NDEGE: Unapochagua airport kama sehemu unayotaka kupeleka abiria ni muhimu kuchagua eneo sahihi lenye watu wengi wanaoelekea kupanda ndege.
Mfano mzuri ni karibu na hoteli kubwa, unaweza kupaki gari kariakoo au posta karibu na mahoteli yenye wageni wengi na hapo uweke destination yako kuwa airport. Ukifanya hivi safari nyingo zitakazoombwa katika eneo hili utakuwa na uwezo wa kuzipokea wewe kuliko wale ambao hawajaweka destination.
VIWANJA VYA STAREHE: Kama kuna sehemu maarufu ya starehe au kama kuna tukio kubwa kama tamasha basi weka destination ya eneo hilo. Baada ya hapo tafuta maeneo yaliyochangamka ambayo unadhani watu wengi watakuwa wanatokea huko kuelekea kwenye tukio.
APPARTMENT ZA KISASA: Kuna safari nyingi unazoweza kupata ukiegesha gari karibu na appartments kubwa na kuset destination ya eneo ambalo lina tukio au lenye sehemu ambazo watu wengi wa mtaa huo hupenda kwenda.
Je ulikuwa unafahamu kuhusu kipengele hiki katika app yako ya dereva UBER? Jaribu kuchagua maeneo unayoyapendelea kwa kutumia destination filter na ufate dondoo za kupata safari nyingi kisha tushirikishe experience yako.